RAIS Samia Suluhu Hassan, amesema makundi ya wawekezaji yanayowasili nchini, ni matokeo ya ziara zake katika mataifa ya nje na kusisitiza kuwa mafanikio hayo yasingepatikana endapo angekaa ofisini.
Aidha, aliwataka Watanzania kumuunga mkono katika juhudi zake hizo, akifafanua kwamba ameamrishwa na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kufanya kazi hiyo.
Rais Samia aliyasema hayo jijini Dar es Salaam Desemba 06, 2021, wakati wa hafla ya kuzindua Kiwanda cha Kutengeneza Vifaa vya Umeme cha Elsewedy Electric East Africa Limited, kinalomilikiwa na mwekezaji kutoka Misri.
Alisema serikali yake itaendelea kuzunguka na kuwashawishi wawekezaji kuja kuwekeza nchini kwa sababu ndiyo wajibu wa kiongozi.
“Nafanya hivi kwa sababu Ilani imenituma katika nafasi niliyonayo kuna muongozo wa kazi sitautimiza kwa kukaa ofisini, Dodoma au hapo wapi… Magogoni, lazima nizunguke, nitoke, nikaonane na watu niongee niwashawishi kwa lugha nzuri waje kwetu,” alisema.
Aliwataka Watanzania kuwapokea vizuri wawekezaji ili waingie nchini kujenga ustawi wa uchumi na kuzalisha ajira.
Alisema jambo la pili linalomsukuma ni kutokana na ukweli kuwa kiongozi ana maswali ya kujibu kwa Mungu, hivyo juhudi zake zinalenga kumfanya asikose la kujibu siku atakapoulizwa.
Rais Samia alisisitiza safari ya kupokea wawekezaji inaendelea na hivyo wananchi waiunge mkono kwa kutoa huduma nzuri ili waendelee kuja.

Aidha, aliwataka watendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji na taasisi zake kuhakikisha wanatumia fursa ya wafanyabiashara 111 waliowasili nchini kutoka Misri angalau nusu yao wawekeze Tanzania.
Aliwasihi kuacha kufanya kazi kwa mazoea na kasi ya utendaji wao iendane na idadi ya wawekezaji na huduma zitolewe kuendana na ukubwa wao.
“Ndani ya ugeni huu kuna wawekezaji wakubwa 40, nitashangaa kuona wanarudi huku wakikosa maeneo ya kuwekeza tuwaeleze na kuwashawishi walau nusu yao wabaki,” alisema.
Alitaka urasimu kuendelea kupunguzwa na mambo kuboresha maeneo mengine ili kuvutia zaidi.
Alisema serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji na kuboresha sheria na sera ili zitabirike na zisibadilike mara kwa mara.
Rais Samia alieleza kufarijika baada ya kuona kundi hilo la wawekezaji ikiwa ni kabla ya kukamilika mwezi mmoja tangu akutane na kuzungumza nao nchini Misri.
Kuhusu kiwanda hicho, alisema ni kikubwa kuliko vyote Kusini mwa Jangwa la Sahara na kitawezesha Tanzania kuuza bidhaa nje ya nchi na kuingiza fedha za kigeni.
Alieleza kiwanda kitazalisha mita 100,000 za nyaya na Transoma 15,000 kwa mwaka na kwamba uwekezaji huo ni kielelezo sahihi fursa nyingi zilizopo nchini.
Alisema mbali na mambo mengine kiwanda hicho kitapunguza utegemezi wa kuagiza bidhaa kutoka nje na badala yake chenyewe kitauza bidhaa nje ya nchi.
Aliema serikali imedhamiria kuhakikisha biashara zinazoanzishwa, zinalelewa na kukua ndani na nje ya nchi, hivyo hapana budi kuimarisha uratibu na kuainisha chagamoto zote za biashara ili kuzitafutia ufumbuzi.
Kuhusu changamoto za barabara Kigamboni, alisema serikali yake itatoa kipaumbele katika huduma wilayani humo kwa kuwa ameifanya kuwa ya viwanda.
Alipongeza mpango wa mwekezaji huyo kujenga chuo kitakachofundisha Watanzania namna ya kufanya kazi ili waajiriwe katika kiwanda hicho.
Alibainisha serikali inaendelea na mpango wake wa ujenzi wa Chuo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na muda wowote jengo linaanza kujengwa.
Aliongeza pia inaendelea kujenga vyuo vya ufundi na hivyo itaangalia fani zipi zifundishwe zaidi kulingana na mahitaji yaliyopo.
Aliema siku chache zijazo taifa litatimiza miaka 60 tangu lipate uhuru na hivyo sherehe hizo zitumike kutathmini utekelezaji wa vipaumbele vya taifa.
Katibu wa NEC ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka, alisema uzalendo wa Rais Samia kwa taifa si wa kutilia shaka.
Alisema kiongozi ninuthubutu, karama, ujasiri na kiongozi huyo ametekeleza ilani kwa ufanisi.
Kuhusu safari za nje ya nchi, Ilani imempa hayo mamlaka ikimtaka kuhuisha na kudumisha diplomasia ya kimataifa.
Aliwahakikishia watanzania kwamba kwa kasi hiyo kufikia 2025 Ilani ya CCM itakuwa imetekelezwa kwa asilimia 100.
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji, Geoffrey Mwambe, alisema Rais ameamua kusherehekea maadhimisho ya miaka 60 ya uhuru kwa uzinduzi wa miradi.
Alifafanua kuhusu ziara ya Rais Samia kwenda Misri imekuja na matunda ya wafanyabiashara wakubwa 40 wanaohitaji kuwekeza kwa kuanzisha viwada 40 nchini.

Alisema tangu Tanzania ipate Uhuru miradi 11,978 imesajiliwa na katika kipindi cha miezi sita ya Rais Samia imesajiliwa miradi mingi zaidi.
Mwambe alifafanua juhudi hizo za serikali zinalenga kutengeneza fursa nyingi za ajira, vyanzo vya mapato na kuondoa utegemezi wa uagizaji bidhaa nje ya nchi.
Alisema mbali nakiwanda hicho mwekezaji huyo ameahidi kuifanya Tanzailnia kuwa eneo lake la pili la kuishi baada ya Misri na kwamba anahitaki kuwekeza katika miradi saba yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni tatu.
Alieleza mchakato wa upatikanaji ardhi kwa ajilii ya mwekezaji huyo unakaribia kukamilika.
Naye Mkurugenzi wa kiwada hicho, Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hicho, Mhandisi Ibrahim Kamal, alisema watatoa mafunzo kwa watanzania kuhusu uzalishaji wa nyaya na transfoma ili kuwaajiri kiwandani hapo.
Alisema kiwanda hicho kitatoa huduma Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makalla, alisema barabara ndiyo kero kubwa katika Wilaya ya Kigamboni na kwamba serikali imetoa sh. bilioni 3.2 kwa ajili ya kutatua chagamoto hiyo.
Aliongeza sh. bilioni tisa zimepelekwa kwa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), kwa ajili ya kushughulika na barabara na madaraja Kigamboni.
Alieleza katika kipindi kifupi tangu Rais aingie madarakani visima sita vya maji vimechimbwa wilayani humo na vitasambaza maji hadi Mbagala.
Na JUMA ISSIHAKA