UMOJA wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Mkoa wa Njombe umesema upo bega kwa bega na Rais Samia Suluhu Hassan ukimuahidi kuwa utahakikisha anarejea tena madarakani Mwaka 2025 ili kuendelea na majukumu yake ya kulijenga Taifa.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mwenyekiti UWT wa Mkoa huo, Scholastika Kevela, amesema wao kama wana Njombe kaulimbiu yao inasema ‘Samia mitano tena’ wakiamini kuwa tangu aingie madarakani miezi nane iliyopita ameonyesha uwezo wa kutosha wa kuliongoza taifa.
Amesema pamoja na kuwa kumeibuka ‘chokochoko’ kutoka kwa baadhi ya viongozi zenye nia ya kutaka kumvunja moyo kiongozi huyo mkuu wa Chama Cha Mapinduzi na Taifa, siyo kwao bali pia hazimtetereshi kiongozi huyo mkuu wa nchi kuwatumikia watanzania.
“Tupo pamoja na kiongozi wetu Rais Samia Suluhu Hassan, ukweli yeye ni kiongozi mchapakazi… muda mfupi wa uongozi wake tangu aingie madarakani ameonyesha uwezo mkubwa wa utendaji kiasi cha kumfanya atambulike duniani kote, hatupo tayari kuona mtu yeyote anamsema vibaya kwa jambo lolote” amesema Scolastika.
Amesema kama viongozi hao walidhani kuwa suala la nchi kukopa ndiyo ajenda kwao ya kumtoa ‘kwenye Reli’ Rais Samia, watambue kuwa kwa hilo ‘wamekosea namba’ wajipange kwa jingine kwa kuwa hakuna taifa lolote duniani lisilo kopa hivyo siyo kitu cha ajabu kwa Tanzania kukopa kwani suala hilo huwezesha kupatikana kwa maendeleo.
Awali akizungumza Januari 04, 2022, wakati akipotea taarifa ya matumizi ya fedha za Uviko -19 Rais Samia Suluhu Hassan alisema inashangaza kuona mtu na akili zake akihoji kuhusu tozo na mkopo wa shilingi trilioni 1.3 kama vile ni jambo la kwanza kutokea Tanzania wakati limekuwepo tangu nchi ilipopata uhuru.
Aliongeza, “ Mtu na akili yake anakwenda kusimama ana argue (kuhoji) ni akili yake na uhuru wake lakini mtu mnayemtegemea kuwa mtashirikiane naye katika safari ya maendeleo hutegemei atasema hicho na hasa kwa sababu bajeti zote masuala yote kiuchumi ndani ya nyumba yake ndio zinapita. Lakini ni 2025 fever wasameheni,”
Aidha, akizungumzia hilo Mwenyekiti huyo wa UWT Mkoa wa Njombe Scholastika Kevela ameungana na Rais Samia na kusema kilichowakuta watu hao ‘Presha’ ya uchaguzi ujao, suala alilowataka kufikiria na kujipanga kwa nafasi zingine kwa kuwa kiti cha Urais tayari kina mwenyewe aliyepo madarakani hivi sasa.
Na MWANDISHI WETU



























