
Njombe;
Mwalimu wa kiume aliyejulikana kwa jina moja la Ngoitanile anayekaribia kuwa na umri wa miaka stini (60) anayefundisha katika shule ya msingi Mwembetogwa iliyopo Mtila kata ya Matola halmashauri ya mji wa Njombe, amekamatwa na polisi kwa tuhuma za ukatili wa kuwaingiza vidole sehemu za siri watoto watano wanaosoma darasa la kwanza na la tatu na kuharibu usichana wao.
Kamishna msaidizi wa polisi mkoa wa Njombe ambaye pia ni kaimu kamanda Butusyo Mwambelo amethibitisha kukamatwa kwa mtuhumiwa mara baada ya kupata taarifa za uficho na kwenda kumkamata mwalimu huyo.
“Bahati nzuri tulikuwa na majina ya wale watoto ambao wako watano, wawili ni darasa la kwanza na watatu ni wa darasa la tatu kwa hiyo tukafanya utaratibu wa kuwapeleka hospitali na dakatari akatoa taarifa kwamba hao watoto inaonekana sehemu zao za siri wameingiliwa na kitu butu hawana bikira” amesema kamanda Mwambelo
Amesema mara baada ya taarifa hizo walilazimika kuwahoji watoto hao juu ya vitendo walivyofanyiwa ambapo waliweka wazi kuwa wamekuwa wakiingizwa vidole sehemu za siri na mwalimu huyo wakiwa darasani huku wakati mwingine akiwaita ofisini.
“Kibaya zaidi walipoulizwa wanafunzi wengine nao walikiri kwamba huyu babu anafanya kitendo hicho mbele ya wanafunzi na lile darasa kuna watoto wa kiume na watoto wa kike,kwa hiyo huyu mwalimu yupo hapa kituo cha polisi lakini ushirikiano kwa walimu tumekosa, wamesema hizo taarifa hawana ila watoto ndio wamesema” ameongeza Kamanda.
Kamanda Butusio ametoa wito kwa wananchi wa Mkoa wa Njombe kuacha kuficha taarifa za matukio kama hayo na kutoa ushirikiano kwa polisi huku pia akibainisha kuwa kwa sasa upelelezi unaendelea dhidi ya mtuhumiwa na hakuna dhamana itakayotolewa kwake kwa sasa mpaka Mahakamani lakini sio kwa jeshi la polisi.



























