LUSAKA, Zambia
SERIKALI ya Zambia imetangaza utaratibu wa mazishi ya mwili wa mwasisi wa taifa hilo, Kenneth Kaunda, aliyefariki dunia Juni 17, mwaka huu.
Makamu wa Rais wa nchi hiyo, Inonge Wina, amesema utaratibu huo unaanza kesho, Juni 23, mwaka huu kwa mwili kuzungushwa katika mikoa 10 ili kuwapa fursa wananchi kutoa heshima zao za mwisho.
Amesema wakati mwili huo ukiagwa, taifa litaendelea kuwa katika maombolezo ya siku 21 na kituo cha taifa cha televisheni kitarusha moja kwa moja matukio yote.
Makamu huyo wa Rais wa Zambia, amesema msafara wa mwili wa Kaunda utapita katika makao makuu ya mikoa pekee.