SERIKALI ya Tanzania imeingia Mkataba wa makubaliano na Taasisi ya Global Health Catalyst ya nchini Marekani kwa ajili ya ujenzi na uanzishwaji wa Kituo cha Umahiri wa Matibabu ya Saratani hapa nchini.
Tukio hilo limeshuhudiwa mbele ya Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Mapinduzi ya Zanzibar Dk. Hussein Ali Mwinyi, Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu pamoja na Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Mhe. Hassan Hamis Hafidh pamoja na Watalaam na Wadau wa Sekta ya Afya Jijini Dar Es Salaam.
Akizungumza katika tukio hilo, Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema Serikali itaendelea kuboresha na kujenga miundombinu ya vituo vya afya pamoja na kuweka mikakati inayolenga kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wote ili kuimarisha kinga na Tiba ya Maradhi ya Saratani.
“Maradhi ya Saratani ni ugonjwa unaoathiri mamilioni ya watu kote ulimwenguni, hivyo kama jamii tunapaswa na sisi kuwekeza katika kinga na tiba ya maradhi haya, tayari Serikali imeanza kuchukua hatua na tunashuhudia hatua katika ujenzi wa miundombinu ya huduma za afya na mikakati inayolenga kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za matibabu kwa wote” amesema Dk. Mwinyi.
Dk. Mwinyi ameongeza kuwa uwekezaji katika huduma za Saratani nchini unakusudia kujenga matumaini ya maisha kwa watu na familia ambazo zimekubwa na changamoto hiyo.
“Lengo la Serikali ni kuhakikisha kila mtu anaekutana na changamoto ya Saratani anapata huduma kamili na matibabu stahiki, Maono ya Mhe. Rais Dk. Samia yanalenga mbali na kuzingatia maendeleo endelevu ikiwemo matumizi ya nishati mbadala kukuza uhifadhi wa mazingira na kuhakikisha matumizi sahihi ya rasilimali zetu za asili, malengo haya yanaonesha dhamira ya dhati ya kutunza mazingira kwa ajili ya kizazi cha sasa na cha baadae, juhudi hizi ni sehemu ya Mkakati wa kukabiliana na ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo saratani” amesema Dk. Mwinyi.
Aidha Rais. Dk. Mwinyi akatumia fursa hiyo kuhimiza juu ya umuhimu wa ushirikiano utakaosaidia kutimiza malengo ya nchi na kuhakikisha upatikanaji wa matibabu bora kwa wagonjwa wa Saratani.
“Kwa kupitia ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi, watafiti na wataalam wa tiba tunaweza kubadilisha kabisa taswira ya huduma za saratani, tuwe na dhamira ya dhati ya kufanya kazi bila kuchoka katika kukabiliana na ugonjwa wa Saratani ili kuleta matumaini kwa wale watakaopata changamoto hio ya kiafya” amesema Dk. Mwinyi .
Kwa upande wake Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu ametoa wito kwa Watanzania kuchukua tahadhari juu ya ugonjwa wa Saratani kwa kuwa kila mwaka wagonjwa wa Saratani Elfu 40 wanagundulika ambapo inapelekea vifo Elfu 26 hivyo Watanzania wasipochukua tahadhari vifo vitokanavyo na ugonjwa huo vitaongezeka.
“Wagonjwa wanaofika hospitali ni asilimia Thelathini tu, wagonjwa wengi wapo mitaani na wanashindwa kufika katika vituo vyetu vya kutolea huduma za Afya, tunawaasa Watanzania kufika katika vituo hivyo na kupata matibabu ya Saratani ili tupunguze wagonjwa pamoja na vifo.” Amesema Waziri Ummy.
Aidha, Waziri Ummy amesema kupitia mradi huo wa kuanzishwa kwa kituo cha huduma za Saratani nchini kutasaidia kupunguza gharama za kupeleka wagonjwa nje ya nchi na muda wa matibabu kwa wagonjwa.
“Nikiangalia takwimu zetu kwa mwaka 2021/22 wagonjwa 89 waliopelekwa nje ya nchi tumetumia Tsh: Bilioni 4.8 na kwa wagonjwa Saratani pekee imetumika Tsh: 3.1 Bilioni, lakini pia kufuatia kituo hiki tutaongeza huduma za tiba utalii (wagonjwa kutoka nje kuja kutibiwa Tanzania).” Amesema Waziri Ummy.
Pia amesema, zaidi ya asilimia 80 ya wagonjwa wa Saratani wanaofika hospitali hali zao zinakuwa katika hatua ya Tatu hadi hatua ya Nne hali ambayo inapelekea kupata ugumu wa matibabu tofauti na ambavyo angewahi kujua hali yake na kuanza matibabu mapema.
“Nitoe wito kwa Watanzania wapime Saratani angalau mara moja kwa mwaka kwa kuwa Saratani inayoongoza ni ya mlango wa kizazi kwa asilimia 25, matiti asilimia 10, tezi dume asilimia 9, mfumo wa chakula asilimia 6.5 na Saratani nyinginezo.” Amefafanua Waziri Ummy.
