SIKU moja baada ya serikali kupiga marufuku utaratibu wa shule za msingi na sekondari kuwazuia wanafunzi kwenda likizo na kusoma hadi usiku katika muda wa ziada, Chama cha Wamiliki wa Shule Binafsi Tanzania (TAPIA), umetoa tamko kuhusu agizo hilo.
Akizungumza na UhuruOnline, Mwenyekiti wa Chama hicho, Mahmoud Mringo, amesema kwa kuwa serikali imetoa maelekezo hayo wajibu wao ni kutekeleza.
Alipoulizwa watachukua hatua gani kuhakikisha shule zote binafsi zinatekeleza agizo hilo, Mringo alisema jukumu la usimamizi ni la mamlaka za serikali, hivyo watatekeleza maelekezo.
“Tumesikia maelekezo ya Waziri, kwa kuwa yeye ndiye msimamizi wa sera na sheria akielekeza tunatekeleza, suala la usimamizi si jukumu letu ni la mamlaka za serikali,” alieleza kwa ufupi.
Wakati Mringo akitoa maelezo hayo, baadhi ya wadau wa elimu walisema shule zilichukua hatua hiyo kwa utaratibu wa kuomba kibali kwa Kamishna wa Elimu kutumia muda wa ziada kufundisha wanafunzi wa madarasa yanayokaribia kufanya mtihani, lakini baada ya agizo la serikali, wanalazimika kutekeleza maelekezo hayo.
Akizungumza, Mkuu wa Shule ya Sekondari St. Anne Marie Academy jijini Dar es Salaam, Gradius Ndyetabula, alikiri kuwepo wanafunzi kusoma hadi usiku na baadhi kutokwenda likizo, lakini kwa madarasa yanayokaribia kufanya mitihani.
Alisema katika shule anayoiongoza wamekuwa wakiwapa mazoezi wanafunzi kwa mujibu wa maelekezo ya Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).
Mkuu huyo alifafanua kuwa, mwaka huu TAMISEMI ilitoa mwongozo unaotaka mwanafunzi akae shuleni kwa siku 192 tu.
Alibainisha utaratibu waliokuwa wakitumia ni kuandika barua za kuomba kuongeza siku chache kwa ajili ya kuwafanyisha mazoezi wanafunzi wa madarasa yanayokaribia kufanya mitihani.
“Waziri ametoa maelekezo na yeye ndiye msimamizi wa shughuli hizi, tunachosubiri ni maelekezo rasmi yatakayoshushwa kwa viongozi wa chini kuanza utekelezaji, lakini tumepokea na tutatekeleza,” alisema.
TAMISEMI YAFAFANUA
Akifafanua agizo hilo, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Profesa Rizik Shemdoe, alisema kupitia marekebisho ya Sheria ya Elimu ya mwaka 1978, zilitungwa Kanuni za Elimu za mwaka 2002.
Alisema sheria na kanuni hizo zinaweka idadi ya siku za masomo kwa mwanafunzi katika mwaka wa masomo husika, kuwa ni siku 194 kwa Shule za Msingi na Sekondari ukiondoa Jumamosi, Jumapili, sikukuu za umma na likizo.
Profesa Shemdoe alisema maagizo hayo yanapaswa kusimamiwa kikamilifu na Ofisi ya Rais TAMISEMI, ambayo ndiyo yenye jukumu la kutekeleza maelekezo ya Kisera na Sheria.
“Kanuni hizo hazikuacha ombwe katika usimamizi, zimeeleza endapo siku za masomo zitapotea kwa sababu zilizo nje ya udhibiti wa shule au mamlaka
“Shule au mamlaka hiyo itapaswa kuomba kibali cha kufidia siku hizo kwa Kamishna wa Elimu na katika kibali chake Kamishna ataeleza muda wa kusoma wakati wa likizo. Hiyo ni kwa shule zote za serikali na binafsi,” alisema.
Alisema Wizara imefanya hivyo kwa kutambua likizo ni muda wa mtoto kupumzika na hivyo kuwa na uwezo wa kufuatilia masomo vizuri zaidi katika muhula unaofuata.
Alisema muda wa likizo humwezesha mtoto kuwatembelea na kuchangamana na ndugu, jamaa na marafiki na hivyo kukuza stadi zisizokuwa za kitaaluma.
“Watoto wetu ni zao la jamii tusijaribu kuitenga elimu na jamii. Pia, tuwape watoto wetu fursa ya kujifunza shughuli ndogo ndogo za kijamii na kiuchumi kama vile usafi wa mazingira, kilimo, upishi, ujenzi na ujasiriamali,” alisema.
Katibu Mkuu huyo, alizitaka shule zote za serikali na binafsi kuhakikisha zinazingatia sheria hiyo.
MADAKTARI WAFUNGUKA
Akizungumza na Uhuru, Rais wa Chama cha Madaktari (MAT), Dk. Shadrack Mwaibambe, alisema ratiba zinazomnyima mtoto likizo na muda wa kupumzika zina athari kiafya na maendeleo ya mwanafunzi.
“Kwa mfano watoto wa darasa la sita wanaoingia darasa la saba mwakani wanaambiwa waende shuleni saa 11 alfajiri, maana yake anaamka saa 10, akitoka hapo anaingia katika programu za kawaida za shule hadi saa tisa na nusu na baadaye saa 10 jioni anaingia darasani hadi saa mbili usiku,” alisema.
Alisema utaratibu huo huwaingiza watoto katika msongo wa mawazo kwa kuwa hawana uwezo wa kulalamika, lakini ukweli wanachoka.
Dk. Mwaibambe alisema hatua ya wanafunzi kulimbikiziwa masomo bila mapumziko huwafanya kuwa na uwezo wa kukariri badala ya kuelewa kwa kuwa wanakuwa na mzigo mzito wanaolazimika kuuhifadhi badala ya kuelewa.
“Hii ndiyo sababu leo hii watoto wetu hawawezi kufanya wanachosoma ingawa wanaweza kupata alama ‘A’ katika mitihani yao, unakuta mtoto amefaulu vizuri lakini ukimleta katika utendaji wa alichosomea anashindwa,” alisema.
Alisema ratiba hizo huwafanya watoto kukosa muda na familia zao na hivyo kushindwa kujifunza mambo mengine muhimu nje ya taaluma za shuleni.
Rais huyo wa MAT alisema madhara mengine yanayomkumba mtoto iwapo atakosa muda wa likizo au mapumziko ni kudumaa kwa maendeleo ya ubongo.
Alifafanua kwamba maendeleo ya ubongo wa mtoto hutokana na kuona, kusikiliza na kugusa hasa kwa watoto wadogo zaidi.
Dk. Mwaibambe alieleza watoto wa shule walishavuka hali ya kugusa na iliyobaki kwao ni kuona na kusikia ambapo hatua ya kukaa saa 14 na nusu shuleni akisikiliza na kuona vitu vya aina moja hufanya ukuaji wa ubongo wake ulemae.
“Mtoto hawezi kupata maendeleo ya ubongo kwa kusikia na kuona jambo moja wakati wote, tunajua nyuma ya hili kuna biashara lakini muhimu wapate mazingira tofauti, hasa wakati wa likizo ambao huutumia kutembelea ndugu na jamaa zao,” alisema.
Alishauri hata utaratibu wa wanafunzi kukaa bweni uwe hiari, wasilazimishwe kama inavyofanywa na baadhi ya shule hasa binafsi kwa madarasa ya mitihani.
Alisema zipo faida nyingi za mtoto kukaa nyumbani na familia yake, kwani nje ya taaluma za shuleni anafunzwa stadi za maisha.
Alifafanua hatua ya MAT kutaka kuanza utafiti wa madhara yanayowakumba wanafunzi kwa kukosa likizo na muda wa kupumzika imetokana na malalamiko ya baadhi ya wazazi.
Alisisitiza wanaendelea kukusanya maoni na baadaye wataomba kukutana na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako, ili kuzungumza naye.
Hata hivyo, UhuruOnline, ilibaini utaratibu huo haufanywi na shule binafsi pekee, bali zipo baadhi ya shule za serikali huwanyima wanafunzi likizo zikiwataka kuendelea kubaki masomoni huku zikiwatoza fedha.
Kauli ya Wazazi
Wakati wadau wa elimu wakitoa maoni hayo, mzazi wa mwanafunzi wa shule binafsi ya Jijini Dar es Salaam (jina tunalo), alisema anaunga mkono kauli ya serikali kuhusu watoto kupata muda wa kupumzika wakati wa likizo.
Mzazi huyo ambaye aliomba hifadhi ya jina lake, alisema mtoto wake anaingia darasa la saba Januari, mwakani lakini shule hiyo imewataka wazazi kulipa sh. 150,000 kwa kila mwanafunzi.
“Naunga mkono kauli ya serikali kukataza masomo ya ziada. Hapa kuna mchezo unafanyika kwa kutumia kigezo cha kuwaandaa watoto wa darasa la saba, lakini kwanini tunalipishwa sh. 150,000 kwa mwezi mmoja tu ambao watakuwa shuleni wakati tuna mzigo wa ada ya Januari inatusubiri,”alihoji mzazi huyo.
Juzi Waziri wa TAMISEMI, Ummy Mwalimu, alitangaza marufuku kwa shule za msingi na sekondari nchini, kuwapa kazi wanafunzi wakati wa likizo, akitaka wapewe nafasi ya kupumzika.
Kauli ya Waziri Ummy imekuja ikiwa ni siku kadhaa tangu Chama Cha Madaktari (MAT), kutangaza kuanza utafiti wa athari za kiafya kwa wanafunzi wanaolimbikiziwa kazi kwa muda wa ziada na kubeba mabegi makubwa.
Na JUMA ISSIHAKA





























