SPIKA wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, amesema katika uongozi wake amedhamiria kuufanya mhimili huo kuwa daraja baina ya serikali na wananchi katika kusimamia utekelezaji wa ahadi za maendeleo.
Aidha, amesema hakuna tofauti iliyopo ya wingi wa idadi ya wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika uendeshaji wa vikao vya Bunge, tofauti na munkari uliokuwepo kutoka kwa wabunge wa vyama vya upinzani, ambao haumaanishi ndio uwakilishi bora kwa wapigakura bungeni.
Akizungumza katika mkutano wake na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari, uliofanyika katika ukumbi wa Msekwa, jijini Dodoma, Dk. Tulia amesema wananchi ndio wenye mamlaka ya kuchagua wabunge, hivyo uwepo wa wabunge wengi kutoka CCM ni kwa sababu wananchi wamewachagua.
Dk. Tulia alisisitiza kuwa katika uongozi wake ndani ya Bunge, amedhamiria kulifanya Bunge kuwa daraja kati ya serikali na wananchi.
Alibainisha wananchi wanapaswa kuwasilisha hoja zao bungeni kupitia wawakilishi wao kisha serikali kutekeleza ahadi ilizotoa kwa wananchi, ambapo Bunge litasimama kama chombo chenye kusimamia utekelezaji wa ahadi za maendeleo kwa wananchi.
Katika mkutano huo, Dk. Tulia aliulizwa endapo uwepo wa idadi ya wabunge wengi kutoka chama tawala kwamba kumeathiri uendeshaji wa Bunge.
Akijibu swali hilo, alisema shughuli za Bunge zinaendelea kama kawaida hakuna tofauti na mabunge mengine yaliyopita, kwa kuwa ndani ya Bunge kinachoangaliwa ni namna gani mbunge aliyechaguliwa na wananchi anavyotekeleza majukumu yake ya kuwatumikia wapiga kura wake.
Alisema wananchi ndio wenye maamuzi ya kuwachagua wawakilishi wao bungeni, hivyo uwepo wa wabunge wengi kutoka Chama Cha Mapinduzi ni kwa sababu wananchi wamewachagua kuingia bungeni.
“Sijaona tofauti ya uwakilishi wa wananchi bungeni, labda tofauti iliyopo ni munkari na kuwa na munkari huko sio kuwawakilisha wananchi. Uwepo wa wabunge wengi wa chama kimoja hadi sasa sioni shida yeyote,”alisisitiza Dk. Tulia.
WABUNGE 19 WA CHADEMA
Akijibu swali kuhusu uhalali au uharamu wa wabunge 19 wa viti maalumu kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuendelea kuwepo bungeni, Spika Dk. Tulia alisema uharamu haupo kwa sababu haiwezekani mbunge kuwepo bungeni wakati hana uhalali wa kuwepo ndani ya chombo hicho kwa kuwa nchi inaendeshwa kidemokrasia na kwa kuzingatia sheria za nchi.
ADHABU KWA WABUNGE
Miongoni mwa maswali yaliyoulizwa katika mkutano huo baina ya Spika na wahariri wa vyombo vya habari ni kuhusu kama kuna kanuni inayoruhusu wabunge wanaofanya makosa kutangazwa kwa wananchi huku akiagiza waletwe katika Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, wakiwa wamefungwa pingu na adhabu za kutohudhuria vikao vya wabunge kuonekana kama inawaumiza zaidi wananchi na sio wabunge.
Akijibu maswali hayo, Dk. Tulia alisema hakuna kanuni ya Bunge inayotaka wabunge wanapofanya makosa watangazwe kwa wananchi.
Hata hivyo, alisema endapo mbunge akifanya makosa inatakiwa taarifa itolewe na wakati mwingine taarifa hiyo inatoka wakati ambao vikao vya Bunge vikiwa vinaendelea.
Kuhusu wabunge kufungiwa kuhudhuria vikao vya Bunge pindi wanapokiuka kanuni, alisema Bunge linaendeshwa kwa mujibu wa kanuni.
Alisema Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, inafanya kazi kwa namna fulani kama mahakama na ndio maana ina mamlaka ya kutoa maagizo ya kukamatwa kwa mhusika pindi akibainika kukiuka kanuni na madaraka ya Bunge.
“Kama spika amesema au hata kama hajasema, lakini aliyeitwa hakuja, atakuwa ameivunjia heshima kamati. Ni lazima atafutwe. Pingu ni lugha ya msisitizo.
“Kuna utaratibu wa kuendesha vikao, kule ndani kuna wabunge 393, ule sio mkutano wa hadhara ni mkutano maalumu kwa shughuli maalumu, lazima ziwekwe kanuni za kuendesha,” alieleza Spika Tulia.
Alisema adhabu kwa mbunge kutohudhuria vikao vya Bunge, inatolewa kwa sababu mwakilishi wa wananchi amekiuka kanuni za Bunge, lakini serikali haisimami kupeleka maendeleo jimboni.
Akizungumzia kuhusu wabunge ambao ni viongozi wa dini, Spika alisema suala hilo ni demokrasia iliyopo nchini ambapo wananchi wana uamuzi wa kumchagua kiongozi wanayemuona anafaa.
SAKATA LA NGORONGORO
Dk. Tulia alisema hoja kuhusu suala hilo tayari kamati ya Bunge imeshatoa mapendekezo kuhusu sakata hilo.
Alisema miongoni mwa mapendekezo hayo ni kuiagiza serikali kufanya utafiti kuangalia matumizi ya ardhi katika eneo hilo na kama kuna changamoto ya masuala ya kisheria, serikali ilete mapendekezo kuhusu mabadiliko ya sheria.
Kuhusu majibu ya uongo bungeni, alisema mhusika pindi akibainika kuzungumza uongo bungeni, atatakiwa kuthibitisha, aombe radhi au kufuta kauli yake na akigoma atatakiwa kuwasilisha ushahidi.
Akijibu swali kuhusu utayari wa Bunge katika kurekebisha vipengele vinavyooneka kuminya uhuru wa habari pindi marekebisho ya Sheria ya Habari yatakapoletwa bungeni, alisema serikali ikiwasilisha suala hilo bungeni, bunge litafanya kazi kwa sehemu yake.
WABUNGE WASIOULIZA MASWALI
Akijibu swali kuhusu kama kuna kanuni inayowabana wabunge wasiouliza maswali au kuchangia mijadala bungeni, alisema hakuna kanuni inayowalazimisha wabunge wasiouliza maswali au kuchangia mijadala bungeni.
“Wabunge hawachaguliwi kwa sababu ya kuuliza maswali wakati maendeleo jimboni hakuna. Wapo wabunge ambao walikuwa wakiuliza maswali sana bungeni, lakini wakati wa uchaguzi hawakuchaguliwa. Hoja kwa wapiga kura wake ni anafanyazi kuwaletea maendeleo wananchi jimboni au la,”alisema Dk. Tulia.
Alieleza kuwa: “Kuna mawaziri hawajawahi kuuliza swali hata siku moja na kila uchaguzi wanachaguliwa, lakini wapo mawaziri ambao hawakuchaguliwa licha ya wao kuwa mawaziri. Hoja ni maendeleo na sio kuuliza maswali.”
BUNGE MUBASHARA
Kuhusu Bunge kuonyeshwa mubashara, Spika Dk. Tulia alisema suala hilo linazungumzika ambapo atazungumza na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye namna ya kulifanyia kazi suala hilo.
“Bunge kuonyeshwa moja kwa moja ni jambo zuri, lakini pia kuna umuhimu kufahamu kwamba sio kila kitu kinapaswa kwenda moja kwa moja,” alieleza.
Akijibu swali kuhusu watu kuwasilisha malalamiko bungeni pindi wanapotendewa ndivyo sivyo na wabunge hususan katika mijadala ndani ya Bunge, kupatiwa nafasi ya kusikilizwa na kutolea ufafanuzi wa suala husika, Dk. Tulia alieleza kwamba jambo hilo lipo kwa mujibu wa kanuni za Bunge.
Alisema mwananchi anaweza kuandika barua ya malalamiko bungeni pindi atakapobaini kutotendewa haki na mbunge katika suala ambalo alilieleza bungeni ambapo baada ya barua hiyo kufanyiwa kazi, mwananchi husika atapatiwa fursa ya kusikilizwa kisha maamuzi yatatolewa.
Akielezea changamoto za uendeshaji vikao vya Bunge, Dk. Tulia alisema kazi ya spika ni kusimamia utaratibu, lakini wapo baadhi pindi uamuzi unapotolewa wanachukulia kwa ujumla kwamba ni uonevu, jambo ambalo sio sahihi.
MWENYEKITI TEF
Akitoa shukrani baada ya Spika Dk. Tulia kumaliza kujibu maswali hayo, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri (TEF) Deodatus Balile, alimuomba Spika kuendelea na utaratibu huo wa kukutana na wahariri na waandishi wa habari.
Hata hivyo, aliomba utaratibu wa mafunzo kwa waandishi wa habari za Bunge urejeshwe kwa lengo la kuongeza weledi kwa waandishi wanaoripoti habari za Bunge.
Kadhalika, aliomba uwekwe utaratibu wa kuwawezesha waandishi wa habari kupata taarifa kuhusu masuala mbalimbali ya Bunge, mapema bila changamoto.
“Kwa waandishi wenzangu wa habari, tuwe makini tunapokuwa bungeni, tuandike habari kwa ujasiri bila uonevu, bila upendeleo na tuzisome kanuni za Bunge,” alisisitiza Balile.
BAKARI MNKONDO Na MUSSA YUSUPH, DODOMA



























