Msimamo wa Chama ni kuwalinda ili wasiyumbe kiuchumi, aidha ni marufuku bodaboda, bajaji kuzuiwa kuingia katikati ya jiji…wenyewe wafurahia wasema chama kimebeba kilio chao.
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimetoa msimamo kuhusu operesheni ya kuwahamisha wamachinga ambapo imewaonya wale wanaofanya kazi hiyo bila kuzingatia maelekezo na maagizo ya Rais Samia Suluhu Hassan.
Kimesema maagizo na maelekezo ya Rais Samia kuhusu wamachinga, ni kuhamishiwa katika maeneo yaliyo bora zaidi yakiwa na miundombinu rafiki ili waendeshe shughuli zao kwa ufanisi.
Chama kimesema kuanzia sasa hakitakuwa tayari kuona kundi hilo la wananchi waliojiajiri likinyanyaswa na kwamba sehemu yoyote kutakapobainika kufanya hivyo chama kitachukua hatua ikiwemo kuzishauri mamlaka za uteuzi dhidi ya mtumishi au kiongozi aliyehusika.
Pia, kimetoa maelekezo mbalimbali ikiwemo kutaka kusitishwa kwa zuio dhidi ya bodaboda na bajaji zisizokuwa za watu wenye ulemavu kuingia katikati ya jiji la Dar es Salaam.
Hayo yalielezwa na Katibu wa Halmashauri Kuuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu msimamo wa chama kuhusu hatua zinazochukuliwa na baadhi ya viongozi katika maeneo mbalimbali nchini.
“Baada ya kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa uamuzi huo wa kisera uliofanywa na serikali, Chama kinaelekeza kwamba, kitendo cha kuwahamisha Machinga bila kuwaandalia maeneo mbadala ambayo yameboreshwa kwa kuwekewa miundombinu kwa ajili ya shughuli zao, ni marufuku na hakikubaliki,” alisema.
Shaka alisema CCM, ndiyo iliyopewa dhamana ya kuongoza nchi na kuunda Serikali baada ya kunadi ahadi na sera zake kupitia Ilani yake ya Uchaguzi ya mwaka 2020 -2025, ambayo kimsingi ndio mkataba kati yake na wananchi.
Alisema moja ya maeneo yaliyopewa msisitizo mkubwa katika ahadi na sera za CCM kupitia Ilani ya Uchaguzi, ni kuongeza ajira, kurasimisha na kuiwekea mazingira rafiki na wezeshi sekta isiyo rasmi.
“Hayo yameelezwa kwenye Ilani yetu ya uchaguzi Ibara za 8(f), 9(F), 32(C), (q) na 122(m). Maelekezo haya ya Ilani yamezingatia ukweli kwamba sekta isiyo rasmi ni sekta muhimu kwa mustakabali wa ustawi wa uchumi hapa nchini, yenye nafasi kubwa ya kutoa ajira, kustawisha maisha ya wananchi na kutokomeza umaskini.
“Aidha, maeneo mengi ya miji nchini ni kitovu cha biashara ambapo wananchi walio wengi wamejiajiri katika sekta isiyo rasmi, wengi wao wakiwa ni vijana na wanawake makundi ambayo ni sehemu kubwa ya wakazi hapa nchini,” alisema.
Shaka alisema huko nyuma iliaminika kuwa, wananchi wengi waliojiajiri katika sekta isiyo rasmi walionekana ni wenye kiwango kidogo cha elimu, lakini sasa wahitimu wengi wa vyuo vya elimu ya juu nao wamejiajiri katka sekta hiyo.
“Hivyo kwa kuzingatia umuhimu wa sekta hii, CCM lazima ibebe wajibu wa msingi wa kulinda maslahi ya wote waliojiajiri hapa,” alisema.
Alisema maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa viongozi na watendaji wa serikali kuhusu kuwapanga upya wamachinga na mamalishe, ni kutumia njia bora bila nguvu ili waendelee kufanya shughuli zao kwa utulivu.
“Mheshimiwa Rais Samia alisisitiza upangaji huo uambatane na wafanyabiashara hao kupewa maeneo ya kufanyia biashara zao Pamoja na kuwekewa miundombinu mizuri. CCM inawapongeza wafanyabiashara wadogo kwa mapokeo chanya kuhusu agizo la Rais Samia.
Kwa mujibu wa Shaka, Chama kimekuwa kikifuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo ya kuhusu wamachinga na kubaini dosari nyingi ikiwemo kundi hilo kutoshirikishwa kikamilifu.
Aliitaja dosari nyingine ni mapendekezo ya wamachinga kutokusikilizwa, maeneo wanyotakiwa kuhamia kutoainishwa, kuhamishwa kimakosa kwa baadhi ya maeneo, matumizi ya nguvu kubwa kiasi cha kuharibu mali, mitaji pamoja na muda uliowekwa kuwa mdogo sana.
APIGA MARUFUKU ZUIO LA BODABODA MJINI
Akizungumzia kuzuiwa kwa waendeshaji wa bodaboda na Bajaji kuingia katikati ya jiji, alisema maelekezo ya CCM kuhusu jambo hilo ambalo utekelezaji wake ulipaswa kuanza leo ni kusitishwa kwa jambo hilo.
“Marufuku ya waendesha/watumiaji wa bodaboda na bajaji kutofika au kutofanya shughuli zao katikati ya jiji la Dar es Salaam si mwafaka, imetolewa bila kuzingatia taratibu za msingi zinazopaswa kutumika kufanya uamuzi unaogusa maslahi ya wananchi, kama huo, hivyo Chama kimeagiza isitishwe mara moja.
Mbali na hilo, Shaka alisema mamlaka za serikali Dar es Salaam, zinazohusisha viongozi, watendaji wa umma, vyombo vya dola na mamlaka zingine zenye majukumu ya kusimamia usafiri na usafirishaji maeneo mbalimbali ya jiji hilo, chini ya Mkuu wa Mkoa (Amos Makala), kwa kuwashirikisha wadau wengine, wakutane haraka iwezekanavyo kuangalia iwapo kuna changamoto zimejitokeza ili zijadiliwe kupata ufumbuzi wa muda mfupi wa kati na muda mrefu, bila kuathiri wala kubugudhi ustawi wa shughuli za makundi ya watu yanayohusika.
“Chama kinasisitiza kuwa, kwa kuzingatia umuhimu wa suala hili, kitafuatilia mrejesho na utekelezaji wake,” alisema.
Alisena kupitia taarifa hiyo, Chama kinaelekeza kuwa amri au maagizo yoyote, yanayogusa maslahi na agenda za wananchi ambazo CCM iliahidi kuzisimamia kupitia Ilani ya Uchaguzi ya Mwaka 2020-2025, yanapaswa kutolewa kwa umma na mamlaka za kamati za ulinzi na usalama katika mikoa na wilaya baada ya suala husika kujadiliwa na kufanyiwa uamuzi katika vikao.
“…Pia ni muhimu kufanya mawasiliano na mashauriano na wadau kwenye nyanja inayohusika,” alisema.
ONYO
Shaka alisema Chama kinaonya kuhusu utaratibu unaoanza kuibuka wa baadhi ya watu kujichukulia mamlaka ya kutoa kauli au maagizo ambayo hayatokani na uamuzi wa vikao ambavyo vimewekewa utaratibu wa kisheria, kulingana na uendeshaji na utendaji kazi wa mamlaka za kamati za ulinzi na usalama za mikoa na wilaya, hali ambayo inaibua sintofahamu na hata chuki katika jamii.
“Chama kinawakumbusha viongozi na watendaji wa serikali kuwa uamuzi wa serikali uliotangazwa na Rais Samia wa kuwapanga na kuwahamisha wamachinga, uliwekewa msisitizo wa kuhakikisha maeneo wanayopangwa au kuhamishiwa yanakuwa yameandaliwa na kuwekewa miundombinu rafiki, kwa ajili ya shughuli za waachinga na wateja wao kuendelea bila kukwamisha fursa za kujitafutia kipato na maendeleo ya kiuchumi kwa ujumla.
Alisema Chama kinafuatilia kwa ukaribu operesheni hiyo katika maeneo mbalimbali nchi nzima.
“Katu hakitakubali wala kuachia liendeshwe kinyume na ilivyoagizwa na maamuzi hayo ya serikali. CCM haitasita kuanzisha hoja au agenda ya kuhakikisha wote wanaokiuka maelekezo ya namna ya kuwapanga Machinga, wanaondolewa katika nafasi zao, kuliko kuwaacha wakizalisha athari hasi katika jamii,” alisema.
Alizitaka kamati za siasa na wilaya na mikoa kufuatilia kwa karibu jambo hilo na kusema popote ambapo utekelezaji wake utakwenda kinyume na maelekezo ya Rais Samia basi nazo zitawajibika.
BODABODA, WAMACHINGA KICHEKO
Shirikisho la Vyama vya Waendesha Bodaboda Dar es Salaam limepongeza hatua hiyo ya CCM kuingilia kati usitishaji wa pikipiki kuingia katikati ya jiji.
Mwenyekiti wa Shirikisho hilo, Said Chenja, alisema walisikitika kwa hatua iliyotangazwa awali na uongozi wa mkoa huo kusitisha pikipiki kuingia mjini.
“Tulisikitika sana. Serikali haiwezi kutuajiri wote. Tunaishukuru CCM kupitia kwa msemaji wake Shaka kwa msimamo huo,” alisema.
Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Machinga Tanzania, Steven Lusinde, alipongeza hatua ya CCM kuingilia kati suala hilo kwani tatizo lililojitokeza siyo wamachinga kutotii maelekezo bali ni baadhi ya maeneo wanayopelekwa kutokuwa rafiki kwa biashara zao.
“Tunakishukuru kwa ujumla wake Chama, kwamba machinga hawana shida na ndiyo maana katika majiji yote waliondoka wenyewe, changamoto inayo kuja ni ya viongozi kulazimisha waondoke wakati hawana pa kuwapeleka katika baadhi ya maeneo. ieIeweke kuwa mmachinga mazingira yake ya biashara ni yawapita njia. Sasa mtu unampeleka Kigilagila atauza nini?”alisema Lusinde.
AGIZO LA RAIS SAMIA
Akilihutubia taifa baada ya kuwaapisha mawaziri wanne na mwanasheria mkuu wa serikali, Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma, wiki kadhaa zilizopita, Rais Samia aliwaagiza wakuu wa mikoa kote nchini, kuliangalia upya suala la wamachinga na kuwapanga upya katika maeneo, wafanyabiashara wadogo maarufu kwa jina la wamachinga.
Pia Rais Samia alitahadharisha kuwa, agizo hilo halina maana utekelezaji wake uhusishe matumizi ya nguvu, mabavu yatakayoleta hali ya kutoelewana baina ya wamachinga, serikali na wafanyabiashara wenye maduka.
“Wito wangu kupitia jukwaa hili, kwa wakuu wa mikoa kuchukua hatua za kuwapanga vyema, na ninaposema kuchukua hatua kuwapanga vyema sitaki kuona yale ninayoyaona kwenye Tv, ngumi, kupigana, kufukuzana, vitu kumwagwa aaah aah,” alisema.
Katika hotuba hiyo, Rais Samia alisema, awali serikali ilitoa fursa kubwa kwa wamachinga kufanya biashara zao kama moja ya njia za kujipatia riziki ya kila siku, hivyo kuipunguzia mzigo serikali.
Na MWANDISHI WETU



























